Sababu ya kumpiga tunayo! Nia ya kumpiga tunayo! Na uwezo wa kumpiga Nduli Idi Amin tunayo, ni lazima tumpige!



Yüklə 0,95 Mb.
səhifə4/18
tarix31.10.2017
ölçüsü0,95 Mb.
#23549
1   2   3   4   5   6   7   8   9   ...   18

***************

Muda mfupi baadaye watu walianza kuondoka na magari yao, Caroline hakuwa na usafiri wa kumpeleka nyumbani kwao, alitamani sana achukue teksi lakini alishindwa kufanya hivyo kwa sababu hakuwa na pesa na pochi yake ilikuwa ukumbini nyuma ya pazia mahali ambako kwa uhakika asingeweza kwenda tena kwa sababu ya aibu aliyokuwa nayo! Alishindwa kuelewa angeondoka vipi ukumbini hapo.

Alisimama nyuma ya mti mkubwa na kuendelea kulia bila kujua cha kufanya, alihisi dunia imemgeuka tena na kuichukua furaha yake! Alijilaumu kuzaliwa na ugonjwa usiopona, aliona ni heri hata uzuri aliokuwa nao usingekuwepo maana ndiyo uliowafanya wanaume wamfuate.

Yakiwa yamebaki magari kama matano kwenye maegesho nje ya ukumbi huo, aliliona gari la Dickson likiingia kwenye maegesho, alijua wazi kuwa walikuwa wamemrudia, Caroline alianza kutembea akilifuata gari hilo alishangaa kumkuta Dickson peke yake ndani ya gari.

“Pole sana Caroline!”

“Ahsante sana kwanini mliamua kuniacha lakini?”

“Ni Richard sio mimi alipatwa na aibu sana na amesema hakutaki tena maishani mwake!”

“Kweli?” Aliuliza Caroline kwa mshangao.

Mambo aliyofanyiwa na Harry yalikuwa tayari yamemrudia tena, maumivu aliyoyasahau yalikuwa yamerejea, alijiona ni binadamu mwenye mkosi kuliko binadamu wengine wote duniani kwa mara nyingine tena uamuzi wa kifo ulianza kumfuata kichwani mwake, alianza kutamani kifo, hakuwa tayari hata kidogo kupambana na aibu iliyokuwa mbele yake, aibu ya kuzomewa sababu ya ugonjwa.

“Lakini nilimwambia Richard kuwa tarehe 26-28 huwa siyo nzuri kwangu akalazimisha!” Alisema Caroline huku akilia.

“Hivi ina maana huwa unaanguka kila mwezi?”

“No! No! No! Nilitaka kusema hivi ....... tarehe hizo huwa si nzuri kwangu!” Alidanganya Caroline lakini alikosa namna ya kuitetea hoja yake na kujikuta akirudia maneno yaleyale.

Sentensi hiyo ya Caroline ilimfanya Dickson aelewe jambo tofauti, hisia kuwa Caroline alikuwa amelogwa zilianza kumtoka na alianza kuamini Caroline alikuwa na kifafa kwa muda mrefu!

“Ulianza lini kuugua?”

“Kuugua nini?”

“Kifafa?”

“Nani kakuambia mimi nina kifafa?”

“Si ulianguka ukumbini?”

“Kwani kuanguka ni kifafa?Mimi sina kifafa Dickson ila nilikunywa dawa za malaria aina ya Halfan halafu sikula chakula zikanizidi nguvu!”

“Ahaa! Pole sana!”

“Ahsante sana lakini unanipeleka wapi Dickson?”

“Ninakupeleka hotelini kwa Richard ukalale au?”

“Nitafurahi sana ukifanya hivyo kwani ninahitaji kumwelewesha Richard kuhusu jambo hili sitaki kukosana naye!”

“Sawa!”

Badala ya kupelekwa Sunshine hoteli aliyofikia Richard, alipelekwa hoteli Bridge side hoteli!



“Na huku tumekuja kufanya kitu gani?”

“Richard alisema nikulete hapa halafu nimfuate!”

“Sawa basi fanya haraka!”

Wote wawili walipanda hadi ghorofa ya tatu kulikokuwa chumba namba 222! Dickson alikaa kitandani na Caroline alikaa kwenye kochi, ilikuwa hoteli nzuri yenye kila kitu ndani!

“Mfuate basi!”

“Subiri dakika chache nipumzike!” Alisema Dickson lakini badala ya kukaa dakika chache alizosema alikaa zaidi ya saa nzima! Caroline alianza kuingiwa na wasiwasi na kumkumbusha tena ndipo alipoondoka na hakurejea tena mpaka masaa matatu baadaye ikiwa tayari saa tisa ya usiku alipoingia chumbani peke yake bila kuongozana na Richard, mkononi mwake alikuwa na kopo kama la dawa ya mbu ya Doom!’

“Yupo wapi Richard?”

“Amekataa kuja! Amesema hana shida na wewe tena na usimfuatefuate!”

“Mungu wangu nitafanya kitu gani mie!” Alisema Caroline huku akilia.

“Lakini usijali sana kama amekuacha poa tu msichana mzuri kama wewe, nipo tayari kumwacha Mariam niwe na wewe!” Alisema Dickson huku akijaribu kumpapasa Caroline kifuani, ni kitendo hicho ndicho kilifanya aielewe nia yake.

“Koma! Nimesema koma na kama umenileta hapa kunifanyia fujo basi umeshindwa, niachie mimi niondoke zangu nikafie mbele!” Aliongea kwa ukali Caroline huku akisimama wima na kuanza kuufuata mlango uliokuwa bado haujafungwa kwa ufunguo.Kabla hajaufikia mlango Dickson alimdaka na kumuangusha chini

“Dickson nitakushtaki na kwa uhakika utafungwa maisha kwa kunibaka!”

Dickson hakujali na bila kusita alilichukua kopo la dawa lililokuwa pembeni yake na kumpulizia Caroline usoni bila kujali kiasi cha madawa aliyopuliza, yalikuwa ni madawa ya usingizi ambayo hutumiwa chumba cha upasuaji kufanya upasuaji.

Caroline alilegea na kuanguka sakafuni Dickson akambeba na kumtupa kitandani kisha kumvua nguo zote alizovaa akabaki kama alivyozaliwa yeye pia alifanya hivyo hivyo.

***************

Nusu saa baadaye kazi aliyodhamiria kuifanya alikuwa ameikamilisha na akili yake ilimrejea na kumkuta Caroline amelala pembeni yake akiwa kimya, alionekana kuwa katika usingizi mzito, hakuelewa kitu chochote kilichoendelea chumbani hapo! Kila alipouangalia uzuri na ulaini wa ngozi ya Caroline kwenye taa Dickson alizidi kuhemuka na hivyo kuzidi kumfanyia ukatili Caroline bila yeye kufahamu.

Mpaka saa kumi na moja alifajiri Caroline alikuwa bado hajazinduka usingizini, Dickson alianza kuingiwa na wasiwasi na hakuelewa angemtoa hotelini na wazo jingine lililomwijia kichwani ni juu ya kifungo kilichokuwa mbele yake, alijua kwa vyovyote baada ya kuzinduka Caroline angeyasema yote yaliyompata na ni lazima angemwingiza Dickson jela!

“No! No! Huyu ni lazima afe kwani nani anajua nipo naye hapa?”Aliwaza Dickson.

Baada ya kuwaza hayo alitoka hadi nje kwenye gari lake ambako alichukua guni tupu alilotumia kubebea mkaa siku moja kabla na kuingia nalo hadi ndani ya chumba, alihangaika lakini hatimaye alifanikiwa kumwingiza Caroline ndani ya gunia hilo akiwa bado usingizini na kutoka akiwa amebeba gunia hilo begani na kwenda kumtupa ndani ya gari lake!

Baada ya kazi hiyo Dickson aliingia katika gari lake na kuondoka kwa mwendo wa kasi akifuata barabara ya Morogoro, aliendesha, nusu saa baadaye na alifika Kibaha! Ambako alikata kulia kufuata barabara iendayo Msata mbele kilometa kama ishirini hivi katikati ya pori alilishusha gunia na kulitupa vichakani!

“Tutaonana ahera!” Alisema Dickson huku akiondoka kurejea mahali alipoliacha gari lake! Kabla ya kuondoka aligeuka na kuliangalia gunia roho ilimuuma kugundua alikuwa amemuua msichana mzuri asiye na hatia.

*************

Dakika ishirini na tano baadaye tayari alikuwa nyumbani kwake akioga na kuvaa nguo safi, hakutaka kukaa nyumbani alitoka kwenda moja kwa moja hadi hotelini kwa rafiki yake Richard, alimkuta akilia machozi.

“Vipi mshikaji?”

“Caroline hajaonekana tangu jana usiku nimemtafuta mno nampenda sana Caroline, yaliyotokea jana yalikuwa ni hasira tu!”

Moyo wa Dickson ulilipuka kwa hofu! Alijisikia mkosaji na hakujua ni kwa jinsi gani angeificha siri aliyokuwa nayo.

“Mbona umeshtuka sana?” Richard alimuuliza rafiki yake.

Dickson alishikwa na kigugumizi.



Je nini kitaendelea? Fuatilia wiki ijayo.

R

ichard alionyesha wazi 
kumkubali Caroline 
pamoja na tatizo alilokuwa nalo, jambo hilo lilimshangaza sana Dickson. Alijua wazi Caroline alikuwa mfu.



“Kwanini umeonyesha mshangao mkubwa kiasi hicho Dickson?”

“Nimeshangaa sana sababu jana tulimwacha palepale nje ya ukumbi sasa atakuwa amekwenda wapi?” Dickson alimjibu Richard huku akitetemeka.

“Hata mimi sifahamu mahali alipo nimemtafuta sana, sehemu pekee ambayo sijafika wala kuulizia ni nyumbani kwao na ninaogopa kufanya hivyo!” Alisema Richard, mwili wake ulijaa hisia kuwa Caroline alikuwa katika matatizo.

“Labda atakuwa nyumbani kwao?” Dickson aliuliza ingawa ukweli aliufahamu

“Kwa kweli sifahamu labda tupige simu!”

“Namba yao ya nyumbani unayo?”

“Ninayo!”

Richard kishujaa kabisa alijikakamua na kunyanyua simu na kupiga namba ya nyumbani kwao na Caroline jibu alilopewa lilimkatisha tamaa zaidi, aliyepokea simu hiyo alikuwa mtoto mdogo na alimtaarifu kuwa baba na mama yake hawakuwepo nyumbani.

“Wamekwenda wapi?”

“Wamekwenda kumfatuta dada!”

Jibu la mtoto huyo lilizidi kumchanganya akili Richard na kumfanya abaki akijilaumu moyoni mwake kwa kitendo kibaya cha kumuacha Caroline ukumbini usiku.

“Nilifanya makosa sana kwani huo ndio ulikuwa wakati wa kumuonyesha Caroline mshikamano zaidi! Nahisi atakuwa amejinyonga au kujiua kabisa na kama itakuwa hivyo sijui mimi nitafanya nini!” Aliwaza Richard huku akionyesha huzuni kubwa, Dickson alimuwekea Richard mkono begani na kumbembeleza.

****************

Kushiriki kwa Caroline katika kinyang’anyiro cha Miss Bongo kulifanywa siri kubwa sana kwa sababu katika tarehe za mashindano hayo zilikuwa ni zile tarehe za hatari kwake ambazo hakutakiwa kutoka nyumbani hata dakika moja.

Ni mpango wa uongo uliofanyika kati ya Mariam Hassan na Caroline ndio ulimwezesha kushiriki mashindano hayo, Mariam alitoka chuoni IFM na kwenda nyumbani kwao Caroline na kumdanganya shangazi yake kuwa alikuwa na sherehe ya kuzaliwa kwake nyumbani kwao na alitaka Caroline awe kwenye sherehe hiyo na wasingechelewa kurudi.

Mara ya kwanza shangazi alikataa katata lakini baadaye Caroline alimwita chumbani kwake na kuanza kumbembeleza akimhakikishia kusingekuwa na tatizo lolote siku hiyo na asingechelewa kurudi nyumbani. Caroline alikuwa tayari kusema uongo wowote ili mradi amridhishe Richard.

“Shangazi kwanza siku hizi sianguki mara kwa mara, mfano mwezi uliopita sikuanguka kabisa! Hizi dawa za Wachina zinanisaidia sana, naomba tu uniruhusu niende shangazi!” Caroline alizidi kumbembeleza shangazi yake hatimaye akakubali lakini akamwomba anywe kwanza dawa na alimwomba Mariam amwachie namba yake ya simu.

“Ahsante sana Mariam bila wewe nisingeruhusiwa!” Alisema Caroline kabla ya kuondoka nyumbani.

“Mbona kuna siku nyingine tarehe 26 inapita bila mimi kuanguka kawnini iwe leo?” Aliwaza Caroline wakati wakipanda ndani ya gari kwenda ukumbini.

****************

Mpaka saa kumi na moja alfajiri Caroline alikuwa bado hajarejea nyumbani! Jambo hilo lilimtia wasiwasi mkubwa sana shangazi yake Caroline, ilikuwa ni mara ya kwanza kwa mtoto huyo kuchelewa nyumbani kiasi hicho, fikra ya kwanza kumwijia kichwani mwake ilikuwa ni kifafa! Alihisi Caroline alichelewa kwa sababu alianguka kifafa katika sherehe aliyokwenda.

“Atakuwa ameanguka kifafa na wamempeleka hospitali lakini kwanini wasinitaarifu? Hebu ngoja kwanza nimpigie simu yule rafiki yake!” Aliwaza shangazi na kuchukua simu ya mkononi iliyokuwa pembeni kwenye meza ndogo na kuanza kubonyeza namba za Mariam sekunde ishirini tu baadaye alisikia simu ikiita.

“Hallow shangazi yake Caroline anaongea sijui ninaongea na Mariam?”

“Ndiyo!”


“Caroline ameamua kulala huko huko nini?”

Mariam alikosa jibu la kumweleza kwani aibu waliyoipata ukumbini ilikuwa kubwa mno na isitoshe kitendo cha kumwacha Caroline ukumbini kilikuwa kibaya zaidi na mpaka wakati huo hakufahamu ni wapi alikokuwa, sababu ya hofu hiyo aliamua kukata simu!

Kukatika kwa simu kulitafsiriwa na shangazi kama ubovu wa mawasiliano na aliamua kupiga kwa mara nyingine! Safari hii simu yake haikupokelewa kabisa.

“Labda simu yake imeishiwa chaji acha nisubiri nitampigia tena baadaye!” Alijisema shangazi yake lakini hata alipojaribu kupiga tena baadaye hali iliendelea kuwa hiyo hiyo.

Hali hiyo ilizidi kumchanganya zaidi shangazi alishindwa afanye kitu gani ili kuwa fahamu mahali aliokuwa Caroline mpaka alfajiri hiyo! Alishindwa kuelewa angewaeleza nini wazazi wake kama angekuwa amepatwa na matatizo yoyote.

Kilipokucha asubuhi bila Caroline kurudi hakuwa na jambo jingine la kufanya zaidi ya kuendesha gari lake hadi chuo cha usimamizi wa fedha kumtafuta Mariam aliyekuja nyumbani kumchukua Caroline, bado aliamini walikuwa wote mpaka asubuhi hiyo.

Aliendesha gari lake kwa mwendo wa kasi akipitia barabara za Ali Khan upanga na baadaye kuingia barabara ya Ali Hassan Mwinyi hadi kwenye mataa ya hoteli ya Sheraton ambako alikata kushoto kuingia mtaa wa Ohio hadi alipokutana na barabara ya Samora, hapo alikata kulia na kunyoosha moja kwa moja hadi chuo cha usimamizi wa fedha.

Aliegesha gari lake na kushuka kisha akatembea kuelekea kwenye lango la kuingilia, alipokelewa na mlinzi na kumweleza shida yake.

“Subiri kidogo nikamwangalie sina uhakika kama amerudi maana jana alikwenda kwenye mashindani ya urembo Diamond Jubilee!” Alisema mlinzi na kuanza kutembea akimwacha shangazi amekaa kwenye kiti akiwa mwenye mawazo mengi.

Neno ‘Mashindano ya urembo’ lililosemwa na mlinzi lilifungua fikra mpya kichwani mwa shangazi, aligundua alichoambiwa jana yake hakikuwa kweli.

“Hivi inawezekana nilidanganywa eh!” Aliwaza mama huyo lakini alishindwa kulikubali wazo hilo moja kwa moja na kuliweka pembeni.

“Kuna mgeni wako nje dada Mariam!”

“Mgeni?”

“Ndiyo!”


“Yukoje?”

“Ni mama mweusi, mnene!”

Maelezo hayo peke yake yalimtosha kueleza ni nani aliyekuwa akisubiri nje, alipochungulia dirishani alimwona shangazi yake Caroline ameketi akiwa amejishika tama. Hakuwa na jibu la kumpa juu ya mahali alikokuwa Caroline, alichofanya ni kuchukua pochi yake na kutoa noti ya shilingi 10,000 akamkabidhi mlinzi.

“Afande huyo mama ananidai, na mimi hivi sasa sina pesa hebu chukua hii mwambie sipo sawa?”

Kwa pesa hiyo aliyopewa neno ‘sawa’ halikuwa gumu kutamkika mdomoni kwa mlinzi.

Mlinzi alirejea getini na kumpa mama jibu kama aliloelekezwa na Mariam.

“Una uhakika hayupo!”

“Asilimia mia tano mama!”

“Nisaidie kitu kimoja basi!”

“Kitu gani mama?”

“Ulimwona Mariam na msichana mmoja mrefu jana?”

“Ndiyo!Waliondoka wote usiku kwenda kwenye Miss Bongo!”

“Kwenda wapiiiiiii?” Shangazi aliuliza kwa mshangao.

“Kwenye Miss Bongo lakini aliporudi hapa alirudi peke yake sijui mwenzake alimwacha wapi!”

“Kweli?”

“Ndiyo!”


“Kwa hiyo kumbe alirudi mbona umenidanganya?”

“Alirudi lakini nafikiri ameondoak tena asubuhi!”

“Basi akija mwambie shangazi yake Caroline alikuja na amesema umpigie simu haraka, sawa kijana?”

“Sawa mama!”

Shangazi yake Caroline aliingia ndani ya gari na kuondoka kurejea nyumbani kwake ambako alitulia akisubiri simu ya Mariam iingie lakini na haikuwa hivyo mpaka saa tatu na nusu, alishindwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kimempata Caroline.

Baada ya kufikiria kwa muda mrefu nini kifanyike hatimaye alifikia uamuzi wa kwenda ofisini kwa Muandaaji wa shindano hilo kujaribu kuulizia mahali alipokuwa mwanae! Wakati mwingine alifikiri labda waandajai waliwapa washiriki mahali pa kulala.

Alikuta makundi ya wasichana wengi wakiwa wamesimama nje ya ofisi hiyo, wengi walionekana miongoni mwa wasichana warembo kwani walikuwa wembamba na warefu! Alipoteremka ndani ya gari lake wasichana wote waligeuka kumwangalia! Walionekana kuongea kitu fulani kwa chini chini lakini katika maongezi neno kifafa lilisikika! Wasiwasi ulianza kuingia.

Wasichana wote walimwamkia akiingia ofisini kwa Muandaaji, ndani alikaribishwa vizuri na kuketi kitini, hakutaka kupoteza muda kwani baada ya salamu alieleza shida yake.

“Baba mimi shida yangu ni ndogo tu!”

“Ndiyo mama!”

“Mtoto wangu Caroline nasikia alishiriki mashindano ya urembo jana ingawa mimi sikuwa na taarifa na mpaka hivi sasa sijui mahali alipo!”

“Kweli mama?”

“Ndiyo!”

“Sijui nianzie wapi kukueleza lakini ukweli ni kuwa Caroline aliibuka mshindi tena kwa pointi nyingi lakini kabda hajakabidhiwa zawadi yake alianguka jukwaani na kuanza kutoa mapovu mdomoni huku mwili wake ukiwa umekakamaa, watu wote walishangaa sana na hatukuelewa kama ulikuwa ni ugonjwa wake siku zote au vipi?

“Hapana!”Shangazi alijaribu kudanganya, alijua tayari aibu imekwishawapata.

“Alipozinduka alitoka jukwaani mbio akiwafuta wavulana alioongozana ukumbuni pamoja na Mariam na kama sikosei vijana hao wanaitwa Richard na Dickson! Hivi unavyotuona tunamsubiri Mariam hapa ili aje achukue zawadi yake ya gari sababu wakati anatajwa alikuwa ameshaondoka!”

Kwa maelezo aliyopewa alijua mwanae hakuwa hai wakati huo, ilikuwa si rahisi kwa Caroline aliyekwishajaribu kujiua siku za nyuma kustahimili aibu hiyo.

“Lakini kwanini walinidanganya? Ni lazima huyo Mariam anajua mtoto wangu alipo!” Aliwaza shangazi yake Caroline wakati akitoka nje.

Hali tayari ilishaashiria tatizo na hakuwa na njia nyingine ya kumpata mtoto wake zaidi ya kutoa taarifa polisi, hivyo alipofika nje aliingia ndani ya gari na kwenda moja kwa moja hadi kituo cha polisi kati ambako alitoa taarifa juu ya kupotea kwa Caroline.

Ni humohumo kituoni ambamo aliliona gazeti la Niambie la siku hiyo likiwa na picha kubwa ya msichana akiwa amelala chali jukwaani huku mdomo wake ukiwa wazi na umejaa mapovu! Ilikuwa ni picha ya Caroline na juu yake yaliandikwa maandishi makubwa:kifafa chamuumbua mrembo Habari hiyo iliandikwa na mwandishi aitwaye Leonard Katunzi,mwandishi maarufu jijini Dar es Salaam.

Maneno hayo yalimfanya shangazi yake alie machozi ndani ya kituo,moyo wake ulimuuma sana kwani ilikuwa ni aibu kubwa mno kwa mtoto wake na alijua tayari gazeti hilo lilishafika Arusha na wazazi wake Caroline walikuwa wamelisoma na si ajabu walikuwa njiani kuja Dar es Salaam.

Kwa habari hiyo gazetini shangazi aliona dunia nzima ilikuwa ikifahamu Caroline alikuwa na kifafa na kama alikuwa hajafa basi alikuwa kati mpango wa kujitoa uhai! Ilikuwa si rahisi kwa Caroline kuliona gazeti hilo na kuendelea kuwa hai.

“Kuna msichana mmoja atakuwa anafahamu mahali mtoto wangu alipo maana yeye ndiye alikuja jana nyumbani kwangu kumchukua!”

“Kweli? Basi huyo ndiye tuanze nae katika upepelezi wetu yupo wapi?”

“Kuna sehemu anasubiriwa ili apewa zawadi yake ya ushindi wa Miss Bongo amepewa ushindi baada ya mwanangu kupatwa na matatizo!” Alisema shangazi ingawa hakuwa tayari kuyataja matatizo yaliyompata Caroline.

“Wapi wanapotoa hiyo zawadi!”

“Ofisini kwa muaandaji wa Miss Bongo!”

“Haya basi twendeni hukohuko tukamsubiri!”

Waliingia ndani ya gari la shangazi huyo na wote waliondoka kuelekea ofisini kwa muaandaji mtaa wa Aggrey Kariakoo, dakika tano baada ya kuwasili ofisini kwa muandaaji, Mariam aliteremka ndani ya teksi nyeupe akiwa na miwani mnyeusi usoni tabasamu lilitawala mdomoni mwake hasa baada ya kuliona benzi limeegeshwa pembeni.

“Nimeuaga umasikini!” Aliwaza Mariam.

Wasichana wote walimshangilia Mariam wakimwita Miss Bongo, wapiga picha walipiga picha nyingi zisizo kwa ajili ya magazeti yao lakini kabla Mariam hajaufikia mlango wa kuingia ofisini maaskari kanzu watatu walimfuata kwa nyuma na kumsimamisha.

“Dada upo chini ya ulinzi halali wa polisi!”

“Nimefanya nini?”

“Utaelezwa kituoni!”

Wasichana wote, waandishi na hata muaandaaji walishangazwa na hatua hiyo! Mariam alipigwa pingu mikononi na kupakiwa ndani ya gari la shangazi yake Caroline na safari ya kwenda kituoni ilianza.

Warembo pamoja na muandaaji walifuata nyuma ndani ya gari jingine hadi kituoni ambako Mariam alitoa maelezo na baadaye kusukumiwa mahabusu! Katika maelezo yake aliwataja Richard na Dickson kama watu waliokuwa naye na ilitolewa amri nao wasakwe.

**************

Pamoja na kujifanya akilia machozi ya geresha Dickson alifahamu kilichotokea, alikuwa amemuua bila hatia yoyote msichana mrembo Caroline baada ya kumpulizia madawa ya usingizi na kumwingilia kimapenzi bila ridhaa yake! Alijua muda si mrefu sana angesakwa na kutiwa mbaroni jambo ambalo kwa hakika hakuwa tayari hata kidogo kupambana nalo! Dickson hakuwa tayari kukaa gerezani.

“Itabidi nitoroke nitakwenda London mpaka tatizo hili limalizike!” Aliwaza Dickson na alitaka kuukamilisha mpango huo mapema iwezekanavyo.

Aligundua mahali alipouweka mwili wa Caroline ndani ya gunia palikuwa wazi na karibu sana na mjini! Hakutaka mwili huo uonekane kwa sababu ungeweza kupimwa na kuonyesha alama zake za vidole na angesakwa kokote ambako angekimbilia na kurejeshwa Tanzania.

“Ni lazima nilihamishe gunia leo hii hii ikiwezekana nilifunge na jiwe na kulizamisha majini!” Aliwaza Dickson, Richard alishangazwa na ukimya aliokuwa nao rafiki yake siku hiyo ilikuwa si kawaida yake.

“Richard ngoja nifike nyumbani kidogo!” Alisema Dickson akisimama wima.

“Usichelewe basi kurudi mshkaji si unajua tena tatizo lililotupata na mimi nakutegemea wewe?”

“Hakuna noma mshkaji nitarudi baada ya muda mfupi nakwenda kubadili nguo tu!”

“Sawa basi!”

Dickson alitoka nje ya hoteli na kuingia ndani ya gari lake badala ya kwenda nyumbani aliliendesha gari lake kwa kasi kuelekea mahali alikolitupa gunia lililokuwa na mwili wa Caroline.

Mita kumi kabla hajafika karibu kabisa na mahali gunia lilipokuwa akiendesha gari katikati ya vichaka alianza kusikia sauti ya msichana akilia na kuomba msaada.

“Nisaidieni nakufa! Nisaidieni nakufa! Ndugu unayepita na gari tafafhali nisaidie!” Ilisema sauti ya msichana aliyelia.

Sauti hiyo haikuwa ngeni masikioni mwa Dickson, alijua wazi ilikuwa ni sauti ya Caroline! Moyo wake ulipiga kwa nguvu na kuruka pigo moja kama Caroline alikuwa hai basi uwezekano wa yeye kuwa katika matatizo na hata kunyongwa ulikuwa mkubwa zaidi.

“Au nimesikia vibaya?”Alijiuliza mwenyewe Dickson na kuzidi kusogea karibu zaidi alishangaa kuliona gunia lilirukaruka na kujinyonga nyonga huku sauti ya msichana ikilia kutoka ndani yake.

“Nisaidie ndugu yangu, nisaidie dada au kaka yangu uliyekuja na gari, nimetupwa hapa na kijana anayeitwa Dickson alinibaka halafu akaja kunitupa hapa ili nife!” Aliendelea kusema Caroline ndani ya gunia bila kufahamu mtu aliyekuwa akimwomba msaada alikuwa Dickson.

Maneno hayo yalimwonyesha Dickson wazi kuwa kama Caroline angepona basi lazima angetaja kila kitu kilichotokea na yeye angekuwa katika matatizo makubwa.

“Ha! Kumbe afadhali nimeamua kurudi huku upo hai? Kwa maneno unayoyasema Caroline hustahili kuishi kabisa ni lazima ufe, utaniletea matatizo makubwa!”

“Dickson kumbe ni wewe?”

“Ndiyo ni mimi na ninakuua ili kukunyamazisha milele!”

“Tafadhali usiniue Dickson, sitasema kitu chochote nisamehe Dickson!”Alisema Caroline kutoka ndani ya gunia.

“Hapana ni lazima ufe!” Alisema Dickson na kuingia ndani ya gari lake na kuanza kulirudisha kinyumenyume! Lengo lake likiwa ni kuligonga gunia hilo na gari mara nyingi mpaka Caroline afe ndio alibebe kwenda kulitupa baharini!

“Dickson tafadhali usiniue kaka yangu sitasema kitu chochote!” Aliendelea kuomba Caroline.

Dickson hakusikiliza maneno hayo alizidi kuijaza gari yake moto kabla ya kuiruhusu kutoka na kwenda kuligonga gunia, hata Caroline aliugundua alitakiwa kuuawa kwa mtindo gani, aliona ni heri angekufa akiwa usingizini kuliko aina ya kifo alichotakiwa kupambana nacho, alisikia gari likipigwa moto na alizidi kulia akimwomba Dickson abadili msimamo.

“Lazima ufe!” Alisema Dickson kwa sauti ya juu, akili yake ilishabadilika hakuwa binadamu tena bali mnyama.

Je nini kitampata Caroline? Dickson atakamatwa? Fuatilia wiki ijayo!

B

aada ya Mariam Hassan 
kutiwa mahabusu 
msako mkali ulianza kuwasaka Richard na Dickson, magari yaliyojaza maaskari yaliondoka makao makuu ya jeshi la polisi kuelekea hoteli ya Sunshine alikofikia Richard! Walifika na kujitambulisha mapokezi na kupelekewa moja kwa moja hadi chumbani kwa Richard!



“Ngo!Ngo!Ngo!”Mlango uligongwa na koplo Kapesa akiwa na bunduki yake mkononi.

“Nani wewe?” Richard aliuliza kutoka ndani.

“Ni mimi aliitikia mmoja wa wafanyakazi wa hoteli hiyo aliyeitwa Naomi.

Richard aliifahamu sauti hiyo na hofu yake ikapungua, alikwenda kwenda moja kwa moja na kufungua mlango wa chumba, Naomi aliingia ndani akiongozana na maaskari watatu wenye bunduki mikononi, Richard alitetemeka mwili mzima kwa hofu alishindwa kuelewa ni kitu gani kilikuwa kimetokea mpaka maaskari waje chumbani kwake.

Alijaribu kulihusisha tukio hilo na kupotea kwa Caroline, lakini alishindwa kupata uhakika.


Yüklə 0,95 Mb.

Dostları ilə paylaş:
1   2   3   4   5   6   7   8   9   ...   18




Verilənlər bazası müəlliflik hüququ ilə müdafiə olunur ©muhaz.org 2024
rəhbərliyinə müraciət

gir | qeydiyyatdan keç
    Ana səhifə


yükləyin